MVUA YAACHA KILIO TANGA


Nyumba zaidi ya 300 zimezama na maji baada ya kukumbwa na mafuriko katika Kata ya Magaoni, hivyo kusababisha wakazi wake kuhama makazi yao.

Tukio lilo lilitokea usiku wa kuamkia jana majira ya saa 7:00 usiku 
baada ya mvua kubwa kunyesha usiku kucha.

Mwenyekiti wa Kata ya Magaoni, Kassim Abdallah, ambaye pia nyumba yake 
imezama, alisema kuwa mvua iliyonyesha usiku wakuamkia jana,
imeacha hasara kubwa kwa wakazi wa kata hiyo kutokana na kuzingirwa na maji, huku mali mbalimbali zikiharibika.


Alisema mvua hiyo ilianza kunyesha wakati huo mpaka saa 2:00 asubuhi, hivyo kusababisha idadi kubwa ya wananchi kukosa mahali pa kuishi, hivyo kuhamia katika shule na wengine kuhifadhiwa kwa ndugu na jamaa zao.


Abdallah alisema kata hiyo ni mpya kwa kuwa mwanzo ilikuwa sehemu ya kata ya Mabawa kabla ya kugawanywa.

Alisema sababu kubwa ya mafuriko hayo ni kukosekana kwa mifereji ya kutosha, hivyo kushindwa kuruhusu maji kutiririka kwa urahisi.



Mwenyekiti huyo alisema Diwani wa Kata hiyo, 
Mohamed Rajabu, baada ya kuchaguliwa mwaka 2015 alijitahidi kuhakikisha mifereji inajengwa lakini iliyopo haitoshelezi mahitaji ndiyo maana imekuwa rahisi kutokea mafuriko.


Kutokana na athari hiyo, aliiomba Halmashauri ya Jiji la Tanga kutenga fedha kwa
ajili ya mifereji, vinginevyo maafa yanaweza kuwa makubwa zaidi.

Naye Diwani Rajabu alisema mvua hiyo imesababisha 
mafuriko makubwa na kwamba mpaka sasa wananchi hawana mahali
pa kuishi na wamezikimbia nyumba zao huku vyombo vyote vikiwa vimeharibika.



Alisema kuwa ili kuondoa tatizo hilo, alisema ni lazima Halmashauri
ya Jiji la Tanga ipange bajeti kwa ajili ya kutengeneza mifereji ya
kupitisha maji katika kata hiyo, vinginevyo kunawezekana kutokea maafa makubwa
 zaidi.

Comments

Popular posts from this blog

KESI YA ZITTO MUSWADA WA SHERIA YA VYAMA VYA SIASA YAHAMISHWA

Waziri asimamisha likizo za Marubani ATCL