WATU watatu wamefikishwa mahakamani nchini Zimbabwe, wakishtakiwa kuiba mkoba uliokuwa na Dola za Marekani 150,000 (Sh. milioni 345) taslimu mali ya rais wa zamani wa taifa hilo, Robert Mugabe. Washukiwa hao wa wizi wanadaiwa kutumia pesa hizo kununua magari, nyumba na mifugo. Jamaa wa rais huyo wa zamani, Constantia Mugabe, ni miongoni mwa walioshtakiwa, kwa mujibu wa taarifa katika vyombo vya habari vya serikali. Mwanamke huyo anadaiwa kuwa na funguo za nyumba ya kijijini ya Mugabe iliyo eneo la Zvimba karibu na mji mkuu wa Harare, na ndiye aliyewasaidia hao wengine kuingia humo na kufika ulikokuwa mkoba huo. Washukiwa hao wengine walikuwa wameajiriwa kama wafanyakazi wa kufagia na kusafisha nyumbani humo wakati wa kutekelezwa kwa wizi huo siku moja kati ya tarehe 1 Desemba na mapema Januari mwaka huu. “Johanne Mapurisa alinunua gari aina ya Toyota Camry… na nyumba ya $20,000 baada ya kisa hicho,” mwendesha mashtaka wa serikali Teveraishe Zinyemba aliambia ...