Katibu baraza la ardhi kortini


BENJAMIN MASESE
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Geita imehukumiwa Katibu wa Baraza la Kata la Nyamboge, Theleza Barnabas, kifungo cha miaka mitano au kulipa sh 200,000  kila kosa  kwa kupatikana na  hatia  ya kuomba na kupokea rushwa.
Alilipa faini na kuachiwa.
 Akitoa hukumu,  Hakimu  wa mahakama hiyo, Jovith Kato alisema  mahakama ilizingatia ushahidi wa jamuhuri na ushahidi wa utetezi. 
Awali,  Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Dennis Lekayo alidai   Septemba  13, 2018 katika Kata ya Nyamboge  wilayani Geita, mshitakiwa aliomba rushwa ya Sh 200,000 kutoka kwa Sanda Magohe   amsaidie kupata ushindi kwenye shauri la ardhi namba 01/2018 dhidi ya Dotto Maonyole lilokuwa linasikilizwa na Baraza la Kata ya Nyamboge.
Baada ya kuombwa rushwa hiyo,   Sanda ambaye alikuwa ni mlalamikaji katika shauri hilo, aliamua kutoa taarifa hiyo kwa Takukuru Mkoa wa Geita ambako mtego uliandaliwa kwa kutumia fedha za mtego.
Alisema Septemba 20, 2018 Sanda alimpelekea fedha hiyo  mshitakiwa na baada ya kuipokea alitiwa nguvuni na makachero wa Takukuru.
Ilidaiwa   kuwa mshitakiwa siku ya kupokea fedha alimwelekeza Sanda wakutane nyumbani kwake  na  baada ya Maduka kufika kwake mshitakiwa alihoji kama fedha aliyoagizwa imekamilika.
Baada ya kujibiwa kuwa imekamilika, Barnabas alipokea fedha hiyo bila kujua kuwa alikuwa ndani ya mtego wa Takukuru.
 Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Geita, Thobias Ndaro  alitoa wito kwa wananchi  wote wa mkoa  huo  kuendelea kutoa ushirikiano katika mapambano dhidi ya rushwa kwa maendeleo ya mkoa na nchi kwa ujumla.

Comments

Popular posts from this blog

KESI YA ZITTO MUSWADA WA SHERIA YA VYAMA VYA SIASA YAHAMISHWA

Waziri asimamisha likizo za Marubani ATCL