Tabora:Wauguzi wanaotoa lugha chafu waonywa




WAUGUZI na watoa huduma za afya wa zahanati, vituo vya afya na hospitali mkoani Tabora, wametakiwa kufuata maadili ya kazi yao na kuacha kutoa lugha chafu zenye maudhi au kebehi kwa akinamama wajawazito wanaoenda kupata huduma.

Onyo hiyo, limetolewa juzi na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Mkoa wa Tabora, Mwajuma Mhina ambaye alisema baadhi ya akinamama wakiwemo wajawazito wamekuwa wakitendewa ukatili na wauguzi kwa kutolewa lugha chafu afya jambo ambalo ni kinyume na maadili ya kazi hiyo.
Alisema wauguzi kama hao hawawezi kufumbiwa macho kwa kuwa vitendo vya vinadhalilisha utu wa mwanamke na kuwaomba kutoa huduma kwa kuzingatia maadili na misingi ya kazi.
“Huu ni unyanyasaji kwa akinamama, unawezaje kutoa lugha zisizofaa wakati wa mgonjwa akihitaji umuhudumie, umesomea kuwahudumia huo ndiyo wajibu wako utimize.., lakini kwa kuwa wapo wasiosikia tunaiomba Serikali kupitia wizara ya afya kufuatilia na kuwachukuliwa hatua,”alisema.
Alisisitiza UWT ni jumuiya yenye dhamira ya kuwainua akinamama wote ikiwemo kufuatilia changamoto wanazokabiliana nazo iwe kiafya au kiuchumi na kuzifikisha kwa wahusika ili zifanyiwe kazi.

Diwani wa Kata ya Tambukareli, Zinduna Kisamba (CCM), aliunga mkono kauli hiyo na kuwataka waganga wakuu wa wilaya na mikoa kuwachukulia hatua wauguzi wote wenye tabia za namna hiyo ili kukomesha vitendo vya namna hiyo.
Alitoa wito kwa akinamama na wananchi wote kutoa taarifa za wauguzi au wahudumu wa afya wenye tabia za namna hiyo ili hatua za kinidhamu ziweze kuchukuliwa dhidi yao ,ikiwemo kufukuzwa kazi.

Naye Katibu wa UWT mkoani hapa, Hawa Makonyola alisisitiza kuwa serikali ya awamu ya tano ya CCM chini ya Rais Dk. John Pombe Magufuli haina mchezo na watumishi wasio waadilifu, hivyo akawataka kuacha mazoea.

Comments

Popular posts from this blog

KESI YA ZITTO MUSWADA WA SHERIA YA VYAMA VYA SIASA YAHAMISHWA

Waziri asimamisha likizo za Marubani ATCL